SOMA VICHWA VYA HABARI KATIKA MAGAZETI YA LEO OKTOBA 13, 2025

































TFA IMEANZA KUWAUNGANISHA WAKULIMA ZAIDI YA 10,000 NA MASOKO YA ULAYA

 




Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wakulima Tanganyika (TFA)Justin Shirima (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha kuhusu mradi wa kuwaunganisha wakulima na masoko ya kidijitali,(kulia) ni Mkurugenzi wa kampuni ya Defood ya Poland,Adrian Pinko.

Mkurugenzi wa kampuni ya Defood ya nchini Poland (kulia) ,Adrian Pinko akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha kuhusu mradi wa kuwaunganisha wakulima na masoko Barani Ulaya kupitia mfumo wa kidijitali,(kushoto) ni Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wakulima Tanganyika (TFA),Justin Shirima.





Chama cha Wakulima Tanganyika (TFA) kimeanza kuwaunganisha Wakulima zaidi ya 10,000 wa mazao ya kahawa ,parachichi na mazao mengine na fursa za masoko yaliyopo katika nchi za Umoja wa Ulaya hatua ambayo itawapa wakulima uhakika wa soko na kuondokana na changamoto ya ukosefu wa masoko.

Akizungumza na Wanahabari Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wakulima Tanganyika (TFA), Justin Shirima amesema mradi huo ni juhudi za pamoja kati ya TFA na kampuni ya mawasiliano ya kidigitali ya Defood.org yenye makao yake nchi Poland.

“Mradi huu ni mkubwa ambao unaleta majawabu ya masoko ya mazao ya wakulima wa Tanzania kwa wanunuzi wa Ulaya baada ya kufanya kazi na kampuni kwa miaka miwili ya kutembelea mashamba na kuangalia ubora wa mazao tunaanza mradi huu wa Oktoba”,amesema Shirima

Amesema uhakika wa soko ni mkubwa kupitia anwani ya defood.org na unalenga kuwawezesha wakulima kuwasiliana moja kwa moja na wanunuzi wakubwa wa Ulaya wenye maduka makubwa.

Shirima ameongeza kuwa wametembelea wakulima kwenye mikoa ya Arusha na Kilimanjaro ambako wamejionea namna uzalishaji wa mazao ya Parachichi na Kahawa ulivyoshamiri ambayo yamepewa kipaumbele kwa wanunuzi wa mazao ya kilimo Ulaya.

“Niwaombe wakulima hasa wanachama wetu wa TFA watumie fursa hii kwaajili ya kuuza mazao yao,tunaanza kukusanya takwimu kwa wakulima ili tuone wakulima wanaoweza kuzalisha mazao yenye viwango vinavyotakiwa na masoko ya Ulaya kwa kuwakutanisha na kujadiliana nao,”amesema Shirima

Naye Mkurugenzi wa kampuni ya Defood,Adrian Pinko ameahidi kutumia uzoefu alioupata nchini kuwaunganisha wakulima nchini na wanunuzi kupitia mtandao wake unaowaunganisha wakulima ulimwenguni na wanunuzi wa Ulaya.

“Kupitia mfumo wa mawasiliano ya kidigitali tunaweza kuwaunganisha na masoko ya Ulaya kwasababu ninaona fursa kubwa Tanzania kuuza mazao ya kilimo na urahisi kwa masoko ya duniani ambayo ni mazuri,”amesema Pinko

Ameongeza kuwa mradi huo utajumuisha mazao mengi ya chakula yakiwemo pia Nyanya,Mbogamboga na aina mbalimbali za matunda jambo litakaloinua Uchumi wa mkulima mmojammoja.

TAKUKURU YAWAHAMASISHA WENYE ULEMAVU KUJITOKEZA KUWACHAGUA VIONGOZI WANAOWEZA KUTETEA MASLAHI YAO

 




Kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 wa kuwachagua Madiwani, Wabunge na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Morogoro imewahamasisha watu wenye ulemavu kujitokeza kwa wingi kutimiza haki yao ya kikatiba ya kuchagua viongozi wanaoweza kutetea maslahi na maendeleo yao.

Akizungumza wakati akifungua mafunzo ya utoaji elimu dhidi ya rushwa kwa viongozi wa vyama vya watu wenye ulemavu na mahitaji maalum mkoani humo, Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Morogoro, Bw. Christopher Mwakajinga, amesema ushiriki wa kundi hilo katika uchaguzi si hisani bali ni haki yao ya msingi inayotokana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Ushiriki wa watu wenye mahitaji maalum kwenye uchaguzi ni haki ya kikatiba, si fadhila. Ni lazima tuweke mazingira huru na sawa ili waweze kuitumia haki yao ya kupiga kura,” amesema Mwakajinga.


Amefafanua kuwa Katiba ya nchi inatoa haki ya kushiriki katika uongozi kwa Watanzania wote waliotimiza umri wa miaka 18 bila kujali hali zao za kimwili, kiuchumi au kijamii, hivyo ni wajibu wa kila mmoja kutumia haki hiyo kwa uhuru.

Aidha, baadhi ya viongozi wa vyama vya watu wenye ulemavu wamewasihi wenzao wasishawishike na zawadi au rushwa za uchaguzi, bali watumie busara na uelewa wao kuchagua viongozi watakaotetea maslahi ya watu wenye ulemavu, kudumisha amani na kuendeleza maendeleo ya Taifa.